Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu, leo ameongoza kikao cha Kamati ya Uundeshaji Mafunzo ya Epidemiolojia  na Usimamizi wa Maabara (TFELTP), kilichofanyika Dodoma na kuhudhuriwa na Mkurugenzi Mkazi wa Kituo cha Marekani cha Kudhibiti na Kukinga Magonjwa (CDC), Dkt. Mahesh Swaminathan.

Akifungua Mkutano huo, Mganga Mkuu wa Serikali amezungumzia umuhimu wa mafunzo ya Epidemiolojia na Usimamizi wa Maabara Tanzania, na kusisitiza umuhimu wa kutoa mafunzo kwa wataalamu wa afya ngazi zote, ili kuwezesha Taifa kuweza kukabiliana na changamoto ya maradhi ya milipuko pindi yanapotokea ili kuweza kuchukua hatua haraka.

 “Ni muhimu tunapotoa haya mafunzo katika ufuatiliaji na kutilia mkazo elimu sahihi ya ukusanyaji wa taarifa na ufuatiliaji wa magonjwa kwa wataalama wetu ili kama Taifa tuweze kuitikia kwa haraka changamoto za magonjwa ya mlipuko kiulimwengu” Alisisitiza

Aidha amewashukuru na kuwapongeza wafadhili CDC, kwa kuendelea kufadhili mradi mkubwa unaosomesha baadhi ya wataalamu wa Epidemiolojia na kuahidi Wizara kuendelea kushirikiana na wafadhili hao katika kuhakikisha wataalamu wengi zaidi wanazalishwa ili kufikia malengo ya Wizara ya kuwa na Wataalamu wa kutosha wa Epidemiolojia nchini hususani katika mikoa ya pembezoni. Pia, amesisitiza umuhimu wa ufuatiliaji na kuwepo kwa takwimu sahihi za wataalamu wote waliopatiwa mafunzo hayo, ili Serikali iweze kuwatumia pindi kunapotokea changamoto za milipuko ya magonjwa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkazi wa Kituo cha CDC, Dkt. Dr. Mahesh Swaminathan, amesisitiza umuhimu wa Wizara kuanzisha mfumo wa utunzaji taarifa pamoja na machapisho mbalimbali zikiwemo Sera, ambazo ni matokeo ya kuwepo wataalamu wa Epidemiolojia na mafunzo ya Maabara nchini, ili kuwa rahisi  kwa watanzania kufuatilia na kuwepo kwa kumbukumbu za matukio.

Ameahidi kuendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kuhakikisha mradi wa CDC unakuwa na tija na matokeo yaliyokusudiwa kwa Watanzania.

Mkutano wa 14 wa Kamati ya Uongozi ya Mafunzo ya Epidemiolojia na Usimamizi wa Maabara (FELTP) umefanyika katika ofisi za Wizaya Afya, Area D Dodoma na kuhudhuriwa na wajumbe kutoka Wizara ya Afya, Ofisi ya Mganga Mkuu wa Mkoa, Chuo cha Afya Shirikishi Muhimbili (MUHAS), Mashirika yasiyokuwa ya Kiserikali yanayoshughulikia masuala ya Afya, Shirika la Afya(WHO)na Chuo Kikuu Mzumbe watekelezaji wa Mradi wa DCD, Unaofadhiliwa na Serikali ya Watu wa Marekani.

Mkutano huo umeazimia kuongeza wigo wa mafunzo na kuongeza wataalamu Zaidi ili kufikia malengo ya Shirika la Afya Duniani (WHO), yanayotaka katika kila watu 200,000 pawepo na walau mtaalamu mmoja wa Epidemiolojia. Kwasasa Tanzania ina jumla ya wataalamu 892 waliopatiwa mafunzo ya Epidemiolojia na Maabara walioajiriwa katika maeneo mbalimbali ya ndani na nje ya Nchi.

***************************************************************************

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu, akiongoza kikao cha Kamati ya Uendeshaji ya Mafunzo ya Epidemiolojia 

na Usimamizi wa Maabara (FELTP), kilichofanyika Dodoma.

Mkurugenzi Mkazi wa Kituo cha CDC, Dkt. Dr. Mahesh Swaminathan, akikabidhi zawadi ya kanga kwa Mganga Mkuu wa Serikali Prof.

Tumaini Nagu. Zawadi hiyo ni kanga ya maadhimisho ya miaka 20 ya PEPFAR.

Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Nagu akiagana na Mkurugenzi Mkazi wa Kituo cha CDC, Dkt. Dr. Mahesh Swaminathan.

News and Updates

Mzumbe University,
P.O Box 1 Mzumbe,
Morogoro, Tanzania.
Tel: 255 (0) 23 2931220/1/2
Fax: 255 (0) 23 2931216
Cell: 255 (0) 754694029
Email: .
Go to top