Chuo Kikuu Mzumbe kimeendelea kung'ara kwenye jukwaa la kimataifa baada ya kutwaa tuzo mbili za maandiko bora katika Kongamano la 6 la Kimataifa la Utekelezaji na Mnyororo wa Ugavi kwa Afrika (ACOSCM) lililofanyika Bishkek, Kyrgyzstan. Kongamano hilo liliandaliwa na Shirika la Kuehne Foundation na liliwaleta pamoja wataalamu wa ugavi kutoka mataifa mbalimbali barani Afrika.
 
Timu ya Mzumbe iliyoongozwa na Rasi wa Ndaki ya Mbeya, Prof. Henry Mollel, ilishiriki kwa umahiri mkubwa. Bi. Angela Burton Mboma, Mhadhiri Msaidizi wa Ndaki ya Mbeya, aliibuka na Tuzo ya Pili kwa andiko bora na Bi. Sara M. Clavery mhitimu wa Shahada ya Umahiri kutoka Skuli ya Biashara ya Mzumbe, alijinyakulia Tuzo ya Tatu kwa mchango wake mkubwa kwenye tafiti za Ugavi.
 
Ushindi huo umeongeza hadhi ya Chuo Kikuu Mzumbe, ukionesha nguvu ya tafiti zinazofanywa na wahadhiri na wanafunzi wake. Tafiti zilizowasilishwa ziliweza kushindanishwa kimataifa na kuonekana kuwa na viwango vya hali ya juu, hatua iliyosaidia kuleta tuzo hizo nyumbani.
 
Akizungumza baada ya tuzo hizo, Prof. Mollel aliwapongeza washindi na kusisitiza kuwa mafanikio haya yanapaswa kuwa kichocheo kwa wengine kuandika na kuwasilisha tafiti bora zaidi. Alisema kuwa juhudi hizi zinasaidia kuimarisha jina na hadhi ya Chuo Kikuu Mzumbe katika ulimwengu wa kitaaluma.
 
Kongamano la ACOSCM limekuwa likifanyika kila mwaka kwa lengo la kukuza utafiti katika mnyororo wa ugavi. Shirika la Kuehne Foundation linadhamini maandiko bora na kutoa fursa kwa watafiti kuwasilisha kazi zao katika jukwaa hili la kimataifa. Mwaka ujao, kongamano hili litafanyika nchini Afrika Kusini.
Mzumbe University,
P.O Box 1 Mzumbe,
Morogoro, Tanzania.
Tel: 255 (0) 23 2931220/1/2
Fax: 255 (0) 23 2931216
Cell: 255 (0) 754694029
Email: cmu@mu.ac.tz
Go to top