Siku ya Mzumbe na Kambi ya Ujasiriamali 2024 “Mzumbe Day and Entrepreneurship Camp” imefunguliwa rasmi leo tarehe 20 Machi 2024 kwa tukio la Mbio “Funrun” na bonanza la michezo. Ufunguzi huu umeongozwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Mzumbe Prof. William Mwegoha. Siku ya Mzumbe na Kambi ya Ujasiriamali inafanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 20 - 22 Machi 2024 Chuo Kikuu Mzumbe Kampasi Kuu Morogoro.

Tukio hili lenye kaulimbiu “Kuzingatia Teknolojia Zinazoibukia na Njia Mpya za Kujifunza kwa Ajili ya Ukuaji Endelevu” lina lengo la kuibua vipaji na mawazo bunifu ya wanafunzi wa chuo hicho. Pia, tukio hilo litaambatana na mambo kadhaa ikiwemo kutoa nafasi za wafanyakazi na wanafunzi kuonesha ubunifu walionao, kutoa huduma za TEHAMA, huduma za kupima afya, kuchangia damu, msaada wa kisheria, pamoja na kujumuika katika Bonanza la michezo.

Bonanza lilianza kwa kushiriki mazoezi ya viungo, na kufuatiwa na mbio za zilizoshirikisha wafanyakazi na wanafunzi wa mbio za kilometa 5, 10 na kilometa 21 ambapo washindi wa mbio hizo wamepata medali za dhahabu, fedha na shaba na fedha taslimu.

Aidha sambamba na mashindano hayo ya riadha katika kambi hiyo wanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe wanapata nafasi ya kupata mafunzo jinsi ya kuanzisha na kusimamia biashara, upatikanaji wa leseni ya biashara kutoka wakufunzi kutoka Shirika la Viwanda Vidogo (SIDO).

**********************************

 

Mzumbe University,
P.O Box 1 Mzumbe,
Morogoro, Tanzania.
Tel: 255 (0) 23 2931220/1/2
Fax: 255 (0) 23 2931216
Cell: 255 (0) 754694029
Email: .
Go to top